Mabaharia wa KMKM,wamewazabua Kipanga mabao matano kwa moja 5-1 katika mchezo wa muendelezo wa ligi kuu ya Zanzibar kanda ya Unguja uliosukumwa jana jioni ndani ya dimba la Amani mjini Zanzibar.

Katika mchezo huo timu ya Kipanga iliovalia jezi rangi nyeupe, ilionekana kucheza chini ya kiwango, na kuweza kushambuliwa na KMKM mara kwa mara katika lango lao, na ndipo mchezaji Mudrik Muhib alipoanza kupachika bao la kwanza ndani ya dakika ya 19 .
KMKM walizidisha mashambulizi kwa upande wa Kipanga, na wakafanikiwa kuingiza bao la pili lililowekwa kimyani na Faki Mwalim katika dakika ya 25, na baadae Mudrik Muhib akarudi tena wavuni kwa kuingiza bao la tatu mnamo dakika ya 32.
Dakika ya 40 mchezaji wa KMKM Tizzo Charles akazidi kuwakandamiza wachezaji pamoja na wapenzi wa Kipanga pale alipoweza kuifungia KMKM bao la nne 4, na kuzifanya timi hizo ziende mapumziko kwa Mabaharia wa KMKM wawe mbele kwa mabao manne bila ya jibu.

Kipindi cha pili timu hizo zilirudi uwanjani, na Kipanga walionekana kubadilisha mchezo kwa kufanikiwa kufunga bao lililoweka wavuni na mchezaji Amour Suleiman mnamo dakaika ya 52. Kipanga walionekana kwenye safu yao ya ulinzi ktika kipindi cha pili, kwani waliruhusu bao moja tu kwenye lango lao tofauti na kipindi cha kwanza pale Mudrik Muhib alipopiga hatrick kwa kuipatia KMKM bao la tano 5.
Na mchezo huo uliweza kumalizika kwa Kipanga kuchapwa kichapo cha mbwa mwizi cha magoli 5-1.
Katika mechi ya mwisho KMKM walikubali kufungwa bao moja kwa bila walipocheza na Kimbunga, na ndipo walipoamua kulipiza kisasi kwa Kipanga kwa kuwazabua kipigo hicho cha 5-1, huku Kipanga wao mchezo wao wa mwisho walikutana na Miembeni na walitoka sare ya bao 1-1.
Kwa matokeo hayo, KMKM wamepanda hadi nafasi ya tatu (3), wakiwa na alama 23, wakati Kipanga wao wapo nafasi ya kumi (10) na alama kumi na sita (16).
|